UNIDO TAYARI KUSAIDIA TANZANIA YA VIWANDA


Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Viwanda (UNIDO) limesema litasaidia Watanzania kutimiza ndoto za kuwa taifa lenye uchumi wa kati linalotegemea viwanda kwa kuunga mkono utendaji wa pamoja wa sekta ya umma na binafsi.
Kauli hiyo imetolewa katika hafla ya chakula cha mchana iliyoandaliwa na Sekta Binafsi kwa Mkurugenzi Mkuu wa UNIDO Li Yong ambaye alikuwa katika ziara ya kwanza nchini Tanzania na pia ya kwanza nje ya makao makuu ya Shirika hilo baada ya kuchaguliwa kwake kwa mara ya pili mwaka jana.
Alisema katika hotuba yake kwamba moja ya majukumu makubwa ya shirika hilo ni kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu (SDGs)  hasa lengo namba tisa la  maendeleo na teknolojia kwa ajili ya ustawi wa nchi hizo.
Aidha alisema ili kufanikisha hilo kumesisitizwa ushirikiano ambao ni lengo namba 17 la SDGs.
Alisema sekta binafsi ikishirikiana vyema na serikali ndiyo inayoendesha uchumi hasa katika kutoa fursa za kazi kwani asilimia 80 ya kazi kila mwaka hutolewa na sekta binafsi.
Alisema katika hotuba yake hiyo kwamba amefurahishwa na malengo ya Tanzania na nia ya Shirika hilo kuona kwamba malengo hayo kuelekea uchumi wa kati wa viwanda yanatekelezwa kwa kuangalia vionjo muhimu.
Aidha alisema kwamba wataendelea kushirikiana na sekta binafsi kupitia TSPF kuhakikisha kwamba wananchi wanashirikishwa katika malengo ya maendeleo ili kuwa na malengo endelevu na yanayozingatia mazingira.
Naye Mwenyekiti wa Sekta Binafsi nchini- TPSF Dr. Reginald Mengi akizungumza katika hafla hiyo aliitaka UNIDO kusaidia kutengeneza utajiri nchini Tanzania.
Dr. Mengi alisema kwamba ziara ya kiongozi huyo imekuja wakati muafaka, wakati ambapo Tanzania inaelekeza macho yake katika uchumi wa kati na hivyo kuwa na nafasi ya kusaidia ndoto hiyo kufanikiwa.
Alisema wakati nchi nyingi zimekuwa zikipiga maendeleo, zimekuwa na msingi dhaifu wa uchumi wa viwanda kutokana na kusafirisha zaidi bidhaa ambazo hazijasindikwa au zinazotokana na uziduaji.
Alisema hali hiyo pamoja na kuipa utajiri nchi imekuwa haitawanyi utajiri uliopo.
Alisema kutokana na hali hiyo, UNIDO ina kazi kubwa ya kusaidia Tanzania kufikia lengo lake la viwanda hata kusaidia kuanzishwa kwa maeneo ya viwanda (Industrial Park).
Aidha aliishukuru UNIDO kwa kuwezesha sekta binafsi na serikali kukaa pamoja kupitia Baraza la Taifa la Biashara ambako kunakuwa na mazungumzo yenye tija kuhusiana na maendeleo ya biashara na uchumi nchini Tanzania.
Alifafanua kwamba UNIDO ina nafasi kubwa ya kuisaidia Tanzania hasa katika mipango mikakati yake kwa kuunganisha sekta binafsi na umma ili kuiharakisha Tanzania kuelekea uchumi wa kati wenye kutegemea viwanda.
Wakati huo huo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda pamoja na Kimataifa Dr Augustine Mahiga, ambaye wizara yake ndiye ilimwalika Mkurugenzi mkuu huyo, pamoja na kumshukuru kwa kuitikia wito huo aliitakabkusaidia kuchagiza maendeleo ya viwanda.
Alisema kwamba viwanda vya Tanzania bado vichanga na vinahitaji kusaidiwa na kupewa nguvu ya kuendelea mbele kwani pamoja na uchanga wake mchango wake katika kuelekea uchumi wa kati ni mkubwa.
Awali kabla ya hafla ya chakula cha mchana UNIDO ilitiliana saini na serikali ya Tanzania waraka wa kusaidia kuitoa Tanzania katika mipango ya kitaifa kwenda kwenye mipango ya nchi na washirika ili kufikia uchumi wa kati.
Makubaliano hayo yalisainiwa jijini Dar es Salaam kati ya  Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa UNIDO, Li Yong huku yakishuhudiwa na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan.
Share:

No comments:

SIKILIZA JAMII FM

Blog Archive

IDADI YA WASOMAJI

HABARI ZA HIVI PUNDE

HABARI KUU WIKI HII

WAENDESHA BLOG

Contact Form



Recent post