RC TELACK AHAMASISHA WANANCHI KUTOA TAARIFA SAHIHI UTAFITI WA MAPATO NA MATUMIZI YA KAYA BINAFSI

Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Mheshimiwa Zainab Telack amewataka wananchi mkoani Shinyanga kutoa taarifa sahihi kwa watafiti wanaofanya Utafiti wa Mapato na Matumizi ya Kaya Binafsi mkoani humo.

Telack ametoa rai hiyo leo Ijumaa Februari 23,2018 katika mkutano na waandishi wa habari mkoa wa Shinyanga akizungumzia Utafiti wa Mapato na Matumizi ya Kaya Binafsi Tanzania Bara wa Mwaka 2017/2018. 
Utafiti huo unaosimamiwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) unaoendelea nchini katika kata 796 utazifikia kaya 9,552 nchini ambapo kaya 408 zitafikiwa katika kata 34 za mkoa wa Shinyanga. 

Telack alisema njia pekee ya kufuatilia utekelezaji wa program za maendeleo ni kufanya tafiti mbalimbali kama huu unaoendelea ambao unalenga kutoa takwimu za hali ya umaskini na takwimu nyingine ili kuisaidia serikali na wadau kutathmini hatua zilizofikiwa katika kutimiza malengo ya kitaifa. 

“Suala la ukusanyaji wa takwimu rasmi za serikali ni shirikishi na ni wajibu wa kila mwananchi kutoa taarifa sahihi,natoa wito kwa viongozi kuanzia ngazi ya mitaa,vitongoji,vijiji,kata,wilaya na mkoa kutoa ushirikiano wa karibu kwa watafiti watakaozifikia kaya 408 zilichaguliwa katika mkoa wetu”,alisema Telack. 

“Utafiti huu wa Mapato na Matumizi ya Kaya Binafsi Tanzania Bara wa mwaka 2017/2018 unahitaji sana ushirikiano kutoka kwa wananchi wote hasa katika kaya zilizochaguliwa kitaalamu kuwakilisha sampuli za kaya zilizopo mkoani Shinyanga”,aliongeza. 

Alibainisha kuwa kila kaya iliyobahatika kuchaguliwa itahojiwa kwa siku 14 mfululizo na mdadisi atakutana na mkuu wa kaya ambaye hatatakiwa kubadilishwa ili kupata takwimu sahihi kwa ajili kupanga maendeleo ya nchi. 

Mkuu huyo wa mkoa alisema utafiti huo utasaidia kuweka msingi katika kutambua viashiria vya msingi vya kiuchumi,ajira na ustawi wa jamii ambavyo vitatakiwa kufuatiliwa kwa kipindi husika na kupata makadirio ya jumla ya mwenendo wa matumizi ya kaya ili kuandaa fahirisi za bei. 

Telack alizitaja kata 34 za mkoa wa Shinyanga zitakazofanyiwa utafiti kuwa ni Ngokolo,Mwawaza,Ndala,Ndembezi,Songwa,Mwadui Lohumbo,Kishapu,Mwakipoya,Lagana,Talaga,Didia,Mwakitolyo,Iselamagazi,Mwamala,Nyida na Lyabusalu. 

Kata zingine zitakazofikiwa  ni Lyamidati, Lunguya, Chela, ,Jana, Isaka, Chambo, Igunda, Sabasabini, Bulungwa, Ushetu, Ubagwe, Mondo, Nyahanga, Zongomera, Nyihogo,Majengo na Kilago.

Kwa upande wake Meneja wa Takwimu (NBS) wa  mkoa wa Shinyanga, Evarist Tairo alisema huo ni utafiti wa saba tangu nchi ipate Uhuru na utasaidia kwa kiasi kikubwa kupata takwimu halisi za mapato na matumizi ya kaya binafsi.


Share:

No comments:

SIKILIZA JAMII FM

Blog Archive

IDADI YA WASOMAJI

HABARI ZA HIVI PUNDE

HABARI KUU WIKI HII

WAENDESHA BLOG

Contact Form



Recent post