NAIBU WAZIRI DK. NDUGULILE AFANYA ZIARA WILAYA YA SHINYANGA KUKAGUA HUDUMA ZA AFYA

Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile amepiga marufuku dawa za serikali kuonekana zikiuzwa kwenye maduka ya watu binafsi kwani serikali haitaki kuingia kwenye matatizo ya uhaba wa dawa kwenye sehemu zake za kutolewa huduma ya afya.

Dk. Ndugulile amepiga marufuku dawa za serikali kuonekana zikiuzwa kwenye maduka ya watu binafsi wakati wa ziara yake ya kikazi katika wilaya ya Shinyanga, Februari 21,2018 akikagua shughuli za huduma za afya zinavyotolewa kwa wananchi pamoja na kutoa hamasa kwa jamii kujiunga na Bima ya afya ya jamii CHF iliyoboreshwa.
Dk. Ndugulile alisema katika bajeti ya mwaka wa fedha (2017-18) serikali kwenye bajeti ya wizara hiyo ya afya imetenga jumla ya shilingi bilioni 270, tofauti na mwaka wa fedha (2015-16) ambapo zilikuwa milioni 30 hivyo hawatarajii kusikia sehemu za kutolewa huduma zake za kiafya kuwa zina upungufu wa dawa.


Akiwa katika hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Shinyanga na Kituo cha Afya cha Kambarage manispaa ya Shinyanga na kukagua bohari za dawa, Dk. Ndugulile alitoa tahadhari kwa wauguzi kuwa ni marufuku dawa hizo za serikali kukutwa zinauzwa kwenye maduka ya watu binafsi na ikibainika watachukuliwa hatua kali.
“Serikali ya awamu hii ya tano imedhamiria kuboresha huduma za afya hapa nchini, na ndio maana hata bajeti yake imetolewa ni ya fedha nyingi hivyo sisi kama wizara husika hatutarajii kuwepo kwa upungufu wa dawa kwenye sehemu za huduma za afya”,alieleza.
Pia aliwataka wananchi kujiunga na Bima ya afya ya jamii CHF iliyoboreshwa, ili kuwa na uhakika wa kupata matibabu hasa pale watakapougua na kukutwa hawana pesa ambapo wataweza kutibiwa kwa shilingi hiyo 10,000/=  ili kuokoa maisha yao.
Naye kiongozi wa Mradi wa Maendeleo ya Tuimarishe Afya (HPSS) kutoka makao makuu Dodoma Profesa Manoris Meshack, alisema mradi huo wa Bima ya afya ya jamii CHF ulianza mwaka 2011 mkoani Dodoma, na baada ya kufanya vizuri mwaka 2015 ukaongezwa katika mikoa miwili ya Shinyanga na Morogoro.
Alitaja takwimu za kaya katika mikoa hiyo mitatu zilizojiunga na CHF iliyoboreshwa hadi sasa kuwa ni 318,334 sawa na asilimia 26 kati ya kaya 1,220,413, na hadi kufikia Disemba 2017 kupitia uandikishaji wa wanachma wamekusanya shilingi bilioni 7,027,605,547. ambapo shilingi bilioni 2,435,194,000 ni malipo ya tele tele.
Nao baadhi ya wazee kati ya kumi wasiojiweza ambao walikatiwa Bima hiyo ya Afya ya jamii CHF iliyoboreshwa na Naibu Waziri huyo wakati wa ziara hiyo,Mohamed Mkumbola na Regina Kulwa waliipongeza serikali kwa kujali makundi hayo maalumu, na kuomba wazee wote wakatiwe Bima hiyo pamoja na kuendelea kutoa elimu kwa wananchi wajiunge.


Share:

No comments:

SIKILIZA JAMII FM

Blog Archive

IDADI YA WASOMAJI

HABARI ZA HIVI PUNDE

HABARI KUU WIKI HII

WAENDESHA BLOG

Contact Form



Recent post